Sasa ni dhahiri kuwa hali si shwari ndani ya CCM baada ya kujitokeza kundi linalomshinikiza mwenyekiti wake, Jakaya Kikwete kusita kukabidhi chama kwa Rais John Magufuli kabla ya muda wake kumalizika.
Habari zilizopatikana jana mjini hapa zimeeleza kuwa kundi hilo limejipenyeza hadi vikao vya juu vya chama hicho na hasa kile cha Kamati Kuu kilichoketi juzi huku ikidaiwa kuwa linataka Kikwete aendelee mpaka Oktoba mwakani wakati muda wake utakapokwisha.
Vyanzo mbalimbali vililidokeza gazeti hili jana kuwa kutokana na msimamo huo mpya wa kundi hilo, Baraza la Ushauri la Wazee wa CCM linaloundwa na marais wastaafu litakutana kwa dharura muda wowote kujadili, lakini likiwa na mtazamo tofauti. Wazee wanataka mchakato wa makabidhiano wa nafasi hiyo ufanyike haraka.
Wanaounda Baraza la Ushauri la Wazee ni marais wastaafu, Ali Hassan Mwinyi ambaye ni mwenyekiti, Benjamin Mkapa, Amani Abeid Karume na Dk Salmin Amour ambao ni wajumbe.

No comments:
Post a Comment