Lowassa, Mbowe kuongoza kampeni za udiwani CHADEMA


Viongozi wa juu wa Chadema , Freeman Mbowe na Edward Lowassa wataongoza kampeni za uchaguzi  mdogo wa  nafasi za udiwani kwenye kata 43.

Chama hicho kimeunda Kamati za Kitaifa 10, zitakazoongeza nguvu, hamasa na mikakati ya kampeni za uchaguzi wa marudio kwenye nafasi hizo  kuanzia kesho hadi siku ya uchaguzi.

Timu hizo ambazo zitafanya kazi kwa kushirikiana na kamati zingine za hamasa katika ngazi za kanda, mikoa, majimbo, kata na matawi katika maeneo yenye uchaguzi huo, zitaongozwa na Mwenyekiti wa Chama Taifa, Freeman Mbowe.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa chama hicho Tumaini Makene imeeleza kuwa Mbowe  ataanza kuzindua kampeni kesho katika Kata ya Saranga, jijini Dar es Salaam.

Makene ametaja watakaoongoza timu hizo zilizopangwa kwa makundi A hadi G, kuwa ni  Mwenyekiti wa Chama Taifa Freeman Mbowe, Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama na Waziri Mkuu Mstaafu,  Edward Lowassa, Makamu Mwenyekiti Taifa (Bara), Profesa  Abdallah Safari, Makamu Mwenyekiti wa Chama Taifa (Zanzibar) Said Issa Mohamed, Katibu Mkuu wa Chama  Dk. Vincent Mashinji.

No comments:

Post a Comment