MAHAKAMA YAMVUA KENYATTA MAMLAKA KUTEUA JAJI MKUU

Mahakama Kuu ya Kenya imebatilisha marekebisho ya sheria yaliyompa Rais mamlaka ya kuteua Jaji Mkuu kinyume na Katiba, uamuzi ambao umeelezewa na wanasheria wa Tanzania kuwa umechelewa kufanywa hapa nchini.
Wiki iliyopita, majaji watano wa Kenya, Richard Mwongo, Joseph Onguto, George Odunga, Weldon Korir na Mumbi Ngugi walibatilisha mabadiliko ya sheria hiyo, wakisema yanaweka mwanya wa upendeleo, ukabila na hila, gazeti la Metro limeripoti.
Chama cha Wanasheria cha Kenya (LSK) kilifungua kesi hiyo kikipinga mabadiliko ya sheria sehemu ya 30 (3) yaliyofanywa na Bunge Desemba mosi mwaka jana na kusainiwa na Rais Uhuru Kenyatta kabla ya Krismasi, kwa maelezo kuwa yanapingana na Ibara ya 166 ya Katiba.
Mabadiliko hayo yalitaka Tume ya Huduma ya Mahakama (JSC) kuwasilisha kwa Rais majina matatu katika kila nafasi ya watu wanaopendekezwa kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu na Naibu Jaji Mkuu.
LSK ilisema mabadiliko hayo yanaiondolea JSC uhuru wake wa kuteua mkuu wa mhimili huo wa nchi.

No comments:

Post a Comment