Mbowe: Tutakata Rufaa hata kama Sugu ameachiwa Huru

Kufuatia  kuachiwa huru kwa Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi na Katibu wa Chadema Nyanda ya Juu Kusini, Emmanuel Masonga kutoka Gereza la Ruanda, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, amesema bado hawajafahamu ni taratibu gani zimetumika kuwaachia huru wakati  kifungo chao kilikuwa bado.

“Katika mazingira ya kawaida, siku yao ya kifungo walichokuwa wamepewa kilikuwa kinaishia Juni 5, mwaka huu, lakini ghafla wakapewa taarifa kwamba wataachiwa leo. Hatuna hakika sana ni taratibu gani zimetumika kufupisha kifungo chao kwa sababu jambo hilo halijawekwa wazi.

“Tangu wamewekwa gerezani ni takribani miezi mitatu, mawakili wetu walifanya jitihada za kuhakikisha rufaa yao katika mazingira ya dharura inasikilizwa, lakini haikuwahi kupata jaji wala kusikilizwa kwa sababu kila jaji aliyepangiwa kesi hiyo alionekana ana udhuru,”alisema Mbowe.

Aidha, amesema wao wanaamini kesi hiyo haikuwa ya haki kwa sababu watuhumiwa walinyimwa dhamana mwanzoni, na kutokana na mazingira ya kesi yenyewe hawakutakiwa kupewa kifungo. 

Pia amedai kwamba wataendelea na rufaa yao ili kuweka rekodi sawa na kudhihirisha kwamba Sugu na Masonga hawakuwa na makosa.

No comments:

Post a Comment